NENO LA SIKU
Na Mtume na Nabii Josephat Elias Mwingira – Kanisa la Efatha
Tarehe 23/1//2024
Waefeso 6:12 “Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.”
Neno hili linatupa taswila ya wazi kuwa ni katika nani tunapaswa kusimama. Maisha ya mtu ni mbio ya kwenda mbele na sio kurudi nyuma, katika kwenda huko mbele kuna upinzani ukikurejesha nyuma, upi huo? Falme, mamlaka na wakuu wa giza hili, jeshi la mapepo wabaya katika ulimwengu wa roho; haya majeshi ya mapepo wabaya ni hatari mno, unachohitaji ni kufahamu namna ya kuyashinda kwa maana kama usipoyashinda yatakushinda wewe.
Hizo falme, mamlaka na majeshi ya mapepo wabaya yanajua kabisa ya kuwa umepewa nguvu na unayo mamlaka juu yao; yanajua unao umiliki na utawala katika dunia hii, lakini hawataruhusu wewe kufurahia kile ulichopewa na Mungu, ki vipi? Watakufanya ukwame na usiwe na mtembeo, wala mwendelezo wakitumia kutokuitambua mamlaka uliyopewa na Mungu katika dunia hii. Mwana wa Mungu, wewe uliyeokoka umepewa mamlaka ya kumiliki na kutawala katika dunia hii, ukitambua hilo hakuna chochote kitakacho kuzuilia. unapofanyia kazi mamlaka uliyopewa ndipo mbingu inakuwa nyuma yako ili kukusaidia wewe kufikia kule Mungu alipokukusudia.
Tambua mamlaka yako uliyopewa na Mungu na ishi katika hiyo ili upate kuwa mshindi katika ulimwengu huu lakini usipoitambua hiyo mamlaka utaishi kama mhanga, ilihali wewe ni mmiliki wa kila kitu.