NENO LA SIKU
Na, Mtume na Nabii Josephat Elias Mwingira- Kanisa la Efatha
TAREHE: 25/07/2024
Mithali 22:29 “Je! Wamwona mtu mwenye bidii katika kazi zake? Huyo atasimama mbele ya wafalme; Hatasimama mbele ya watu wasio na cheo.”
Usifanye kosa la kumtumikia Mungu kwa ulegevu, maana ndiye aliyekuumba na kuweka ndani yako vipawa na karama kwa ajili ya kumtumikia na kumuabudu. Ni neema kutumiwa na Mungu, maana kuna watu wengine ambao Mungu hawasikilizi japo wanamlilia usiku na mchana. Hivyo, fanya kwa Usahihi, Ukamilifu na Uaminifu maana kila kazi ya mtu italetwa hukumuni. Ukitenda kwa ulegevu, Mungu anakuwekea kongwa la kukukosesha na anaruhusu roho ya upotevu ikujie ili upotee; Mfano: Mfalme Sauli alijikosesha mpaka Mungu akaruhusu roho mchafu aje kwake.
Ili ufikie unapotakiwa, hakikisha wokovu wako sio wa kusukumwa, ongeza bidii na songa mbele daima. Fanya vizuri kwa kutetemeka na kunyenyekea kazi utakayopewa iwe ya Kiroho, Kiakili, Nguvu au ya Matoleo ili upate thawabu kwa Mungu.
Mwana wa Mungu, mtumikie Mungu wako kwa bidii kuonesha unaweza kuaminiwa na Mungu atafungua njia zako.