NENO LA SIKU.
Tarehe: 27/10/2023.
Na Mtume na Nabii Josephat Elias Mwingira.
Isaya 43:26 “Unikumbushe, na tuhojiane; eleza mambo yako, upate kupewa haki yako.”
Usiende mbele za Mungu bila hoja ya kueleweka wala usipeleke malalamiko yako. Katika kila ombi uombalo Mungu amewaandaa Malaika wa kulitekeleza lakini anaangalia Je unachosema kinaendana na Neno?. Usijisahau ukaongea maneno hasi maana yupo mshtaki wetu ibilisi. Kama maombi yako hayajanyooka anayapinga kwa sababu anayo haki ya kufanya hivyo.
Unapoomba kuhusu Ndoa eleza uhalali wako katika Ndoa, kama sio halali maombi yako hayana mashiko, yanakuwa kelele mbele za Bwana. Unapoomba omba kwa imani na kwa ujasiri ndipo utaona matokeo chanya, kukosa ujasiri katika maombi kunatokana na dhambi.
Ni vyema uwe na tabia ya kujifunza Neno la Mungu ili uwe na maombi yenye mguso wa Ki Mungu. Katika maombi yako hakikisha unastahili kupewa hicho unachoomba.