NENO LA SIKU.
Na Mtume na Nabii Josephat Elias Mwingira, Kanisa la Efatha.
Tarehe 16/01/2024.
Isaya 43:26 “Unikumbushe, na tuhojiane; eleza mambo yako, upate kupewa haki yako.”
Usiende mbele za Mungu bila hoja ya kueleweka wala usipeleke malalamiko. Katika kila ombi unaloomba, Mungu amewaandaa Malaika kutekeleza lakini kwanza anaangalia unachosema.
Usijisahau maana pia yupo mshitaki wetu ibilisi, kama mwenendo wako haujanyooka, anayapinga maombi yako kwa sababu anayo haki ya kufanya hivyo. Lakini kama yameombwa kwa Imani na mtu mwenye haki ibilisi hawezi kuyapinga.
Unapoomba kuhusu ndoa, eleza uhalali wako katika hiyo ndoa, kama ni ndoa ambayo sio halali Kibiblia basi maombi yako yanakuwa hayana mashiko; yanakuwa kama kelele mbele za Bwana. Kukosa ujasiri katika maombi kunatokana na dhambi; ni kama mtoto aliyekosea anavyoogopa kumuomba mzazi wake mahitaji yake maana anatambua amemkosea. Maombi ya kinyonge yanatokana na dhambi na kutokufanya sawasawa.
Ni vema kuwa na tabia ya kujifunza Neno la Mungu ili uwe na maombi yenye mguso wa Kimungu. Unapoomba inamaanisha unataka kile unachokitaka kutoka Kwake, maana Mungu ndiye Mpaji; hivyo una sehemu yako Kwake.
Mwana wa Mungu, omba kwa hoja na kwa kumaanisha ndipo utaona majibu ya maombi yako.